Search This Blog

Friday, January 25, 2013

Mapigano makubwa yazuka Moro, Mtwara

• Polisi, wananchi watwangana

MAPIGANO makubwa yamezuka katika mikoa ya Morogoro na Mtwara kiasi cha kusababisha kifo cha mtu mmoja, Mohamed Msigala (60), na kuharibiwa kwa magari na mali nyingine ikiwemo kuchomwa moto kwa mahakama ya mwanzo.

Mapigano yaliyozuka mkoani Morogoro yamehusisha wakulima wa vijiji vya Msolu, Mbigili, Mambengwa na Mabwegere vilivyoko kata ya Dumila, wilaya ya Kilosa, mkoa wa Morogoro, yakiwaacha mamia ya wanawake na watoto wakiyakimbia makazi yao kwa hofu ya kuuawa.

Mapigano hayo yametokea kati ya wakulima na wafugaji wa vijiji hivyo wanaogombea ardhi, inayodaiwa kuuzwa kinyemele kwa baadhi ya mawaziri waandamizi na wafugaji, huku kukiwa na tishio la kufutwa kwa baadhi ya vijiji.

Mali kadhaa yakiwemo magari yameharibiwa vibaya, ambapo nyumba tano za kulala wageni katika eneo la Dumila zimeshambuliwa, wananchi kupora mali mbalimbali zinazodaiwa kumilikiwa na wafanyabiashara wa jamii ya Kimasai.

Mapema majira ya saa 2:30 asubuhi, mamia ya wananchi hao walifanya maandamano kutoka mwanzo hadi mwisho wa mji huo na kutanda kwenye barabara, kabla ya kuiziba kwa mawe na magogo makubwa na kuchoma matairi.

Kikosi cha polisi cha kutuliza ghasia kililazimika kuingilia kati na kupambana na waandamanaji hao kwa mabomu ya machozi na virungu na kufanikiwa kuwakamata idadi kubwa ya wananchi hao.

Pamoja na barabara hiyo ya Morogoro – Dodoma lakini pia wananchi hao walifunga barabara ya Dumila- Kilosa na hivyo kuyafanya magari yaliyokuwa yakitumia barabara hiyo kusimama kwa muda mrefu.

Habari zinasema kuwa vurugu hizo zimechochewa zaidi baada ya wafugaji wa jamii ya Kimasai kuingiza mifugo kwenye mashamba yenye mazao, lakini hakuna hatua zozote zilizochukuliwa licha ya uongozi wa kijiji hadi mkoa kufikishiwa malalamiko hayo.

Mashamba yanayolalamikiwa yako katika eneo la Mabwegere ambalo linadaiwa kuuzwa kwa baadhi ya mawaziri, na hivi karibuni Mkuu wa Wilaya ya Kilosa Elias Tarimo alitangaza kuwa ni mali ya wafugaji jambo ambalo lilipingwa na wakulima.

Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Joel Bendera alilazimika kukatisha shughuli zake za Kibunge huko Dodoma na kurejea mkoani Morogoro kuangalia hali ilivyo.

Hata hivyo, akihojiwa kwa njia ya simu, Bendera alionekana kufura akidai kwamba kulikuwa na upotoshaji mwingi uliochangia kutoeleweka vema kwa suala hilo.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Morogoro, Faustine Shilogile, amethibitisha kukamatwa kwa watu kadhaa katika vurugu hizo na kwamba ulinzi umeimarishwa.

Tuhuma za kuhusika kwa baadhi ya mawaziri katika serikali ya Rais Jakaya Kikwete, huku mmojawao akidaiwa kununua hekari 400, zilianikwa mapema mwezi jana, huku mamlaka zikiwa zinataka kufuta hati miliki ya kijiji cha Mabwegere.

Ilielezwa kuwa watu wasiojulikana waliingia kijijini hapo na kuingilia mipaka na kung’oa alama zilizowekwa na serikali licha ya kuamriwa kuwa mahakama itekeleze zoezi hilo baada ya wanakijiji hao kushinda kesi.

Mbali na kung’olewa kwa mipaka hiyo, watu kutoka maeneo mbalimbali waliendelea kuingia katika kijiji Mabwegere kinyume cha utaratibu na kufungua mashamba ambayo yanadaiwa kumaliza maeneo ya malisho ya mifugo iliyomo kijijini humo. Kijiji cha Mabwegere ni cha wafugaji ambacho ndicho kilichoathiriwa zaidi na machafuko.

Kwa mujibu wa barua yao ya malalamiko, wananchi hao walisema kuwa kwa sasa wamepoteza imani na mkuu wa wilaya na mkurugenzi wao kwani walitegemea kuwa migogoro ya ardhi iliyosababishwa na wakulima kujichukulia eneo la wafugaji ingetatuliwa kwa kuzingatia sheria na utawala bora.

Ofisa mtendaji mstaafu wa kijiji hicho, Sadiki Mwibela, alisema kuwa migogoro mikubwa imekuwa ikitokea kati ya wakulima na wafugaji.

“Kwa sasa msimu wa mvua umeanza, machafuko yanaweza kutokea, lakini mimi kwa kuwa nilikuwa nafuatilia haki za wafugaji waliokuwa wanaporwa mifugo yao kwa kuwa tulikataa kuuza eneo letu, nilifukuzwa kazi, nikakamatwa nikapelekwa jela, nilipotoka nikakuta wameweka mtendaji mwingine,” alisema.

Viongozi wengine ambao waliomba wasitajwe gazetini walisema kuwa walilazimishwa na mkuu wa wilaya kwenda ofisini na kuandika muhtasari ili waziri huyo apewe eneo.

Mtwara hakukaliki

Mkoani Mtwara wananchi wamechoma moto mahakama ya mwanzo na kuharibu gari la polisi, kufuatia kuzuka kwa mapigano kati yao jana.

Mapigano hayo yalianza baada ya askari polisi kuwavamia wananchi katika eneo la Sabasaba waliokuwa wamefurika kushuhudia watu wanaoaminika kuwa wachawi walionaswa usiku wakifanya vitendo vya kishirikina.

Mmoja wa wananchi walioshuhudia tukio hilo, amesema kuwa polisi waliokuwa ndani ya gari wakiwa na bunduki, walifika eneo hilo baada ya kupewa taarifa na msamaria mwema kuwa kulikuwa na vurugu za wananchi waliotaka kuwaua watu hao wawili waliokutwa wakifanya vitendo hivyo vya kishirikina.

Hatua hiyo ya polisi, iliwakasirisha wananchi walioamua kujibu mapigo kwa kuwashambulia kwa mawe na kisha kuharibu gari lao na kulazimika kukimbia kusalimisha maisha yao.

Habari zinasema kuwa askari polisi walirudi wakiwa katika magari matatu na ndipo walianza kuwashambulia wananchi popote walipowakuta katika eneo la soko kuu la Mtwara na kuharibu mali.

Wananchi nao waliamua kujikusanya kwa wingi na ndipo yakazuka mapambano mengine makubwa yaliyosababisha kuchomwa moto kwa mahakama hiyo.

Kamanda wa polisi wa mkoa hakuweza kupatikana, kwa vile simu yake ya mkononi ilikuwa haipatikani kwa muda mrefu.

Polisi waonya

Jeshi la polisi nchini, limewataka wananchi kutii sheria bila shuruti, na wasitumie mwanya wa makosa yanayofanywa na baadhi ya askari au wananchi wengine waliovunja sheria kuhalalisha uvunjaji mwingine wa sheria, kwani makosa mawili hayafanyi haki moja.

Msemaji wa Jeshi la Polisi, Advera Senso, aliiambia Tanzania Daima Jumamosi kuwa ni jambo baya na la hatari ikiwa sasa wananchi wataamua kuchukua sheria mikononi kuvamia vituo vya polisi na kuua askari, au kuvamia mali za watu.

Senzo amelalamikia vitendo vinavyozidi kushamiri nchini kwa wananchi kuvamia vituo vya polisi, kuchoma moto vituo, au wananchi kuacha kabisa kutii amri halali za jeshi la polisi pindi askari wanapofika katika maeneo yenye fujo.

Alikiri kuwa ndani ya jeshi hilo kuna askari wachache wakorofi ambao sio waadilifu, lakini huo sio mwanya kwa wananchi kuhalalisha, kujeruhi au kuvamia vituo vya polisi.

“Tunakataza uvunjaji wa sheria iwe ni kwa askari au raia, ndio maana inapothibitika kuwa polisi amekosea, anachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria za jeshi,” alisema.

Makachero wavamia vyuo

Katika hatua nyingine watu wanaoaminika kuwa makachero wa serikali, wameingia mkoani Mtwara na sasa inadaiwa wanaendesha uchunguzi wa siri wenye lengo la kuwabaini watu wanaotuhumiwa kuwa vinara wa kupinga ujenzi wa bomba la gesi.

Habari za kuaminika zimesema kuwa makachero hao walianza kuwasili mjini hapa, siku sita zilizopita na wamejizatiti katika baadhi ya taasisi nyeti vikiwemo vyuo vya elimu ya juu, kunakoaminika kuwa moto wa hamasa wa kupinga ujenzi huo umeshika kasi.

Mbali na vyuoni, makachero hao wamekuwa wakiendesha uchunguzi katika ofisi za serikali, kujua ni wafanyakazi gani wanaoshabikia jambo hilo na kwamba watakaobainika watakamatwa na kufunguliwa mashtaka mbalimbali yakiwemo ya uchochezi.

No comments:

Post a Comment